Help Children
Love them
Saidia Watoto

Wednesday, March 14, 2012

Kata ya Kipawa yahitaji msaada wa vifaa na fedha kwa ajili ya kufanikisha elimu bora kwa wanafunzi.




Diwani wa Kata ya Kipawa Bonah Kaluwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na matembezi ya kuchangisha fedha kwa ajili ya kuchangia maendeleo ya elimu katika kata hiyo
Mkurugenzi wa Masoko wa Kampuni ya Home Shoping Center Madiha Al Harthy akitoa ufafanuzi kwa waandishi wa habari kuhusiana na tukio hilo.
Home Shopping Center kwa muda mrefu wamekuwa wakisaidia masuala ya maendeleo ya elimu nchini na masuala mengine muhimu katika jamii ya watanzania.


Na Mwandishi wa ElimuBora.
SHILINGI Bilioni moja inahitajika kwa ajili ya kuimarisha miundombinu ya elimu katika kata ya Kipawa iliyopo wilaya ya Ilala, Dar es Salaam.

 Kwa mujibu wa Diwani wa kata hiyo, Bonah Kalua kwa kushirikiana na Manispaa ya Ilala, wameandaa matembezi ya hisani kwa ajili ya kuchangia madawati kwa ajili ya shule zilizopo katika kata hiyo.

Alisema kuwa Kata hiyo inakabiliwa na changamoto mbalimbali lakini kwa sasa wameamua kuanza na sekta ya elimu kwa kuboresha madarasa, vyoo na upatikanaji wa madawati lengo likiwa ni kuhakikisha kila mwanafunzi anapata elimu bora katika mazingira bora.

Kalua alisema kuwa katika matembezi hayo wanatarajia kukusanya sh bilioni moja na kuwataka wahisani na wananchi kujitokeza kwa wingi ili kuweza kuchangia upatikanaji wa madawati ambapo kwa sasa Kata hiyo ina upungufu wa madawati zaidi ya 3,000 katika shule zote.

Aidha alipoulizwa kwamba ni kweli anauchungu na maendeleo ya wananchi wake au lengo lake ni kuvizia Jimbo la Segerea katika uchaguzi ujao, Kalua alisema anachokifanya ni uwajibikaji na anatekeleza wajibu wake kama kiongozi.

Kalua alisema matembezi hayo yaliyodhaminiwa na Home Shopping Center yanatarajiwa kufanyika Jumamosi(Machi 17) kuanzia saa 12 asubuhi katika shule ya msingi Minazi Mirefu na Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mama Salma Kikwete.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Segerea, Dk. Makongoro Mahanga alimpongeza diwani huyo kwa kubuni mikakati ya kuboresha elimu hasa kwa kuchangia madawati ambayo yamekuwa ni kero kubwa.

Pia aliitaka jamii kushirikia kikamilifu katika kuchangia maendeleo yao kwa kuwa serikali pekee haiwezi ambapo pia aliwasihi wananchi wenye uchungu na maendeleo ya elimu kujitokeza katika matembezi hayo na kuchangia chochote

“Kumekuwepo na juhudi za kuongeza madawati na mimi kupitia mfuko wa jimbo nimekuwa nikitenga fedha kwa ajili hiyo... kwa sasa tuna upungufu wa madawati kwa asilimia 40 na kila kata imekuwa ikibuni mbinu na taratibu zake ili kuhakikisha tatizo hili linakwisha” alisema.

Note: Mtandao huu unatoa wito kwa wadau wengine kujitokeza kuungana na HOME SHOPPING CENTER katika kuisaidia kata ya Kipawa 

0 comments:

Post a Comment