Help Children
Love them
Saidia Watoto

Sunday, March 4, 2012

HOTUBA YA WAZIRI WA ELIMU KATIKA MAANDAMANO YA KUCHANGIA MADAWATI.


Mheshimiwa, Meneja Mkuu Msaidizi wa Tigo,
Wawakilishi na uongozi wa Hassan Maajar Trust (HMT),
Timu yote ya Tigo,
Waandishi wa Habari,
Mabibi na mabwana

Ningependa kuwashukuru Tigo kwa kunialika kuunga mkono maswala haya muhimu ya elimu ndani ya nchi yetu.Ningependa kutambua mchango wa Kampuni yenu ya Tigo  katika sekta ya elimu hapa nchini kwa miaka kadhaa sasa.Hii sekta  ina changamoto nyingi sana na serikali inajitahidi sana kupambana nazo.Lakini mzigo ni mzito sana kila mwaka wanafunzi wanaongezeka ambalo ni jambo jema tuu, lakini linaleta mahitaji mengi zaidi.

Nchi yetu ni kubwa sana, tumejitahidi kuwafikia wanafunzi kwenye kila pembe na hata kuaanzisha shule za Kata, ili angalau kila mtoto apate elimu ya msingi.
Shule zetu zinamahitaji makubwa kuliko uwezo wa bajeti yetu, sio siri, kwa hivyo tukipata wadau wanaojali kama Tigo tunafarijiika sana. Ni imani yangu kwamba, serikali pamoja na sekta binafsi inaweza kuleta mabadiliko makubwa kwenye sekta ya elimu ambayo yatakuwa chachu ya maendeleo ya nchi yetu. 
Nimefurahi sana kufahamu jinsi maudhui ya “Tigo Tuchange” yanaendana  na matakwa ya serikali. Jukumu letu ni kuendeleza rasimali kubwa ya taifa letu ambayo ni watu wake. Shule haziwezi kukamilisha jukumu hili peke yake. Walimu hawawezi kukamilisha jukumu hili peke yao. Kinachohitajika sasa ni kama hiki tunachokiona hapa, nguvu ya pamoja ya kutenda kutoka kwa kila mmoja.
Takwimu zinaonyesha kuwa kuna upungufu wa madawati yapatayo milioni tatu nchi nzima, na wanafunzi wengi wa shule za msingi hawanabudi kukaa chini ya miti au kwenye sakafu au vumbi, wakati wa masomo. Elimu bora inaweza kupatikana kwa kuwa na sehemu nzuri ya kusomea pamoja na vifaa vya kujifunzia. Kuwekeza katika elimu sio tu kwa ajili ya mtoto pekee bali kwa ajili ya familia, jamii na umma kwa ujumla. Pia inawezesha uchumi wa kizazi kijacho kunufaika. Tigo imefanya jambo  sahihi kwa kufanya Kampeni hii maalum. Wizara iko pamoja na Tigo , bega kwa bega na itatoa orodha ya shule zinazohitaji madawati, na itashirikiana na Tigo pamoja na HTM kusambaza haya madawati ipasavyo.

Tungependa kuhamasisha makampuni mengine kufuata mfano wa Tigo, ili kuweza kufanya mabadiliko katika maisha ya watoto wetu .


Nawashukuru kwa usikivu wenu, na sasa naomba nitamke kwamba kampeni hii imezinduliwa rasmi


0 comments:

Post a Comment