Help Children
Love them
Saidia Watoto

Sunday, April 14, 2013

Suala la Walimu kupewa kipaumbele katika bajeti hii


WIZARA ya Nchi Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma imesema katika mwaka ujao wa fedha 2013/2014, imedhamiria kuhakikisha kuwa inashughulikia kikamilifu kero za watumishi ikiwemo matatizo ya walimu.

Pamoja na wizara hiyo, Wizara ya Nishati na Madini nayo imebainisha wazi kuwa katika jitihada za kuondokana na tatizo la umeme, asilimia 90 ya bajeti ijayo itaenda kwenye miradi ya maendeleo.

Akizungumza Dar es Salaam jana Waziri wa Utumishi wa Umma, Celina Kombani, alisema katika mchanganuo wa makadirio wa bajeti ya wizara yake vipaumbele vikuu ni kuimarisha mfumo wa taarifa za wafanyakazi pamoja na mishahara yao.

“Mfumo huu tayari umeshaanza kufanyakazi na lengo lake hasa ni kuhakikisha tunaondokana na malimbikizo ya madeni ya mishahara na posho, watumishi na mishahara hewa lakini pia kuimarisha shughuli zote za kiutumishi nchini,” alisisitiza Kombani.

Alisema baada ya mfumo huo ulipoanza mapema mwaka huu ulianza na kuingiza taarifa za walimu 16,000 wapya waliopatiwa ajira mwaka huu ambao wote walipata mshahara wao wa kwanza kwa muda muafaka tofauti na ilivyokuwa zamani.

Aidha alisema pia katika bajeti hiyo inayokadiriwa kuwa ni Sh bilioni 32 kipaumbele kingine ni kuimarisha maslahi ya watumishi wa umma kwa kuangalia upya mazingira wanayofanyia kazi, motisha na mazingira magumu kwa kila kada.

Aidha alisema pia bajeti hiyo imezingatia eneo la kuimarisha tume ya utumishi wa umma ambayo imeongezewa bajeti (hakuitaja) ili kuweza kukagua vyema utendaji wa watumishi wa umma nchini.

“Tume hii pia itaangalia na kuhakikisha inatatua matatizo ya walimu ambayo yamekuwa kero kubwa kwa muda mrefu nchini, ambapo pia safari hii itaimarisha sekretarieti ya ajira kwa kuiongezea kiwango cha bajeti,” alisema.

Alisema pamoja na hayo kwa kuwa wizara hiyo ya utumishi wa umma ni ya muungano, katika bajeti ya mwaka huu, wametenga fedha kwa ajili ya kujenga ofisi za wizara ya utumishi wa umma Zanzibar ili kuhakikisha huko nako masuala ya utumishi na ajira yanafanyiwa kazi vyema.

Kuhusu kiwango cha fedha ambacho wizara hiyo ilipatiwa katika mwaka wa fedha unaoishia baada ya miezi miwili ijayo, Kombani alisema wizara yake imepatiwa takribani asilimia 86 ya bajeti nzima.

Kwa upande wake Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, alisema bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka ujao wa fedha itakuwa ni ya kihistoria kwani haijawahi kutokea dunia kote kwa nchi kutenga asilimia 90 ya bajeti ya wizara ya nishati na madini katika eneo la miradi ya maendeleo.

“Jamani sisi tunachotaka ni kuhakikisha haya matatizo ya umeme nchini tunayamaliza kabisa, ila tunachowaomba watanzania wawe wavumilivu kwa sababu kwa takribani miaka 30 sasa hatukuwekeza kwenye sekta ya umeme ndio maana matatizo mengi yanatakumba,” alisema.

Alisema katika kuhakikisha matatizo yaliyopo yanafanyiwa kazi, asilimia hiyo 90 ya bajeti imewekwa kwenye miradi ya maendeleo na asilimia 10 imeenda kwenye matumizi mengine. “Hakuna nchi yeyote duniani inayotenga katika wizara yake asilimia 90 nzima ya bajeti iende kwenye miradi ya maendeleo,”

Alisema pamoja na bajeti hiyo ambayo hakutaja imetengewa kiasi gani katika makadirio ya mwaka ujao wa fedha, alisema kwa sasa hayuko nchini yuko Norway baadaye ataenda Ubelgiji na Uholanzi ambako amealikwa ikiwa ni jitihada za Serikali za kutafuta fedha za miradi ya maendeleo.

Kuhusu kiasi cha fedha ambacho wizara hiyo imepatiwa katika bajeti inayoishia ya mwaka 2012/2013, Profesa Muhongo bila kutaja kiasi cha fedha walichopata hadi sasa, alisema bajeti ya wizara hiyo imeenda vizuri na kwamba wao kama wizara hawawezi kulalamika.

“Sisi hatuwezi hata kidogo kulalamika hali yetu kiuchumi inafahamika lakini pia bado mwaka haujaisha bado miezi miwili imebaki na bajeti inaendelea kutolewa,” alisema.

Mwisho

0 comments:

Post a Comment