Help Children
Love them
Saidia Watoto

Tuesday, April 16, 2013

Wanafunzi yatima wapewa misaada


WANAFUNZI yatima na waishio kwenye mazingira magumu 80 wilayani Kyela wamepewa msaada wa sare na vifaa mbalimbali vya shule vikiwa na thamani ya jumla ya sh milioni nne.

Shirika la The Struggle for Community Support Alliance(SCSA) lenye makao makuu yake wilayani hapa ndilo lililotoa msaada huo uliokabidhiwa juzi ikiwa ni siku rasmi ya kuzinduliwa kwa mpango mkakati wa miaka mitano wa shirika hilo.

Vifaa vingine vilivyotolewa kwa wanafunzi hao ambao ni wa shule za msingi ni pamoja na daftari na kalamu za wino na risasi huku pia shule ya awali ya Itunge Education Point ya wilayani hapa pia akipewa msaada wa vitabu 20,mbao mbili za kuandikia na makasha ya chaki.

Kwa mujibu wa uongozi wa SCSA, wanafunzi waliopata msaada huo ni kutoka katika kata kumi za wilayani hapa ambazo ni pamoja na Makwale,Ndobo,Ipinda,Kyela mjini,na Ikana.

Kata nyingine ni Ipande,Ngana,Ikimba,Itope na Katumba huku kata nyingine zinazosalia zikitarajiwa kunufaika na msaada kama huo katika awamu nyingine zijazo.

Mkurugenzi mtendaji wa shirika hilo Abraham Mwanyamaki alisema msaada huo ni sehemu ya utekelezaji wa mpango mkakati wa shirika wa mwaka 2013/2017 ambapo zaidi ya bilioni mbili zinataraajiwa kutumika.

Mwanyamaki alisema mpango mkakati huo umejikita katika progamu nne alizozitaja kuwa ni Huduma za elimu,Huduma za afya vijijini,uwezeshaji jamii kiuchumi pamoja na uhifadhi wa mazingira.

“Tunaamini kuwa maendeleo ya wanakyela yataletwa na sisi wenyewe. Ndiyo sababu tumejikita katika kutatua changamoto zilizopo kwenye utekelezaji wa maendeleo wilayani hapa.Tulikwishatoa msaada wa dawati 100 na sasa tunaendelea”

“Tunapenda kuona wanakyela wananufaika na fursa zilizopo kwenye maeneo yao.Lakini pia jamii itambue kuwa utekelezaji wa shughuli za kimaendeleo umekuwa chanzo kikubwa cha uharibifu wa mazingira yetu.Tunataka mambo haya yaende sambamba na utunzaji mazingira” alisema.

Hata hivyo Mwanyamaki alisema utekelezaji wa mpango mkakati wa  SCSA kwa kipindi cha miaka mitano unakabiliwa na changamoto nyingi zinazohitaji ushiriki wa wadau mbalimbali kuzitafutia ufumbuzi.

Baadhi ya wanafunzi waliopokea msaada huo,  Lucia Alphonce na Marium Benson walishukuru shirika hilo kwa msaada wa vifaa vya shule wakisema itakuwa chachu ya wao kujituma katika masomo yao kwakuwa watajiona hawako tofauti na wenzao.
mwisho







0 comments:

Post a Comment